Balozi Dkt. Kanza Ahamasisha Diaspora Kuwekeza Tanzania
- Leo Nzali

- Mar 11
- 2 min read
Updated: Mar 13

Matukio haya yamejiri mwishoni mwa wiki hii jijini Dallas, Texas, katika maadhimisho ya miaka 12 tangu kuanzishwa kwa huduma ya Umoja Prayerline huduma ya maombi kwa njia ya mtandao inayofanyika kwa lugha ya Kiswahili na kuwakutanisha Watanzania na waumini mbalimbali wanaoishi ughaibuni.
Mgeni rasmi katika kongamano hilo alikuwa Balozi wa Tanzania nchini Marekani, Elsie S. Kanza. Akitoa hotuba yake, Mheshimiwa Balozi alitoa wito kwa Watanzania wanaoishi nje ya nchi kuendelea kuwekeza nyumbani Tanzania ili kuchangia maendeleo ya taifa.
“Ningependa kutoa rai kwa wana Diaspora kuendelea kuwekeza nyumbani Tanzania. Serikali ya Tanzania inatambua nafasi muhimu inayochezwa na Watanzania wa diaspora katika maendeleo ya taifa letu. Kupitia uwekezaji mnaoufanya nyumbani kwa njia mbalimbali, mmekuwa chombo muhimu katika kuleta fursa kwa taifa letu, ikiwemo katika biashara, ajira, elimu pamoja na sekta nyingine nyingi zinazowanufaisha Watanzania,” alisema.

Aliongeza kuwa Serikali inaendelea kuthamini mchango huo na kuahidi kuwa Ubalozi wa Tanzania nchini Marekani utaendelea kutoa ushirikiano na msaada kwa Watanzania wa diaspora katika maeneo mbalimbali yanayoweza kuchangia maendeleo ya nchi. Katika hotuba yake, Balozi Kanza pia alisisitiza umuhimu wa amani, uhuru wa kuabudu na uhuru wa kujieleza katika jamii. Alieleza kuwa misingi hiyo imekuwa muhimu katika kudumisha mshikamano na utulivu nchini Tanzania.
Alibainisha kuwa serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, imeweka kipaumbele katika kuhakikisha uhuru wa kuabudu na kudumisha amani nchini, huku taasisi mbalimbali zikiendelea kushirikiana katika kuimarisha misingi hiyo.
Kwa upande mwingine, Ubalozi wa Tanzania uliipongeza Kanisa la Umoja kwa mchango wake wa kuwaunganisha Watanzania wanaoishi ughaibuni kutoka makundi na maeneo mbalimbali kupitia huduma za kiroho na kijamii.

Aidha, Balozi Kanza aliwahimiza Watanzania wa diaspora kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wa dira ya maendeleo ya taifa, Tanzania Development Vision 2050, ambayo inalenga kuelekeza maendeleo ya Tanzania katika kipindi cha miaka 25 ijayo. Alisisitiza kuwa ushiriki wa diaspora katika uwekezaji, biashara, elimu, mafunzo na ushirikiano wa kimataifa utaendelea kuwa nyenzo muhimu katika kuharakisha maendeleo na ustawi wa taifa la Tanzania pamoja na wananchi wake.










Comments